ACHENI KULISHA MIFUGO KWENYE MABONDE YA KILIMO - PINDA

Wednesday, May 13, 2009

12 Mei, 2009

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

ACHENI KULISHA MIFUGO KWENYE MABONDE YA KILIMO - PINDA
*Aonya mifugo kupitishwa barabarani


WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewaonya wafugaji walioko kwenye bonde la ziwa Rukwa waache kuingiza mifugo yao kwenye mabonde ya umwagiliaji kwa vile inaharibu miundombinu katika miradi hiyo.

Alitoa kauli hiyo jana jioni (Jumatatu, Mei 11, 2009) wakati akiwahutubia wakazi wa kata ya Ilemba wilayani Sumbawanga, mkoani Rukwa mara baada ya kukagua skimu ya umwagiliaji ya Sakalilo.

“Katika hali ya kawaida, hili bonde lenye hekta 4,000 siyo la kulisha ng’ombe au mbuzi bali ni la kulima mazao ya chakula, mkiligeuza kuwa la malisho mtakuwa vichaa,” alisema huku akishangiliwa na wakazi hao.

Alisema mifugo ni lazima itengewe maeneo yake ya malisho na kukiri kuwa serikali ilifanya makosa kuruhusu mifugo iingie kwenye mabonde ya kilimo. “Tunatumia fedha nyingi sana kujenga miundombinu halafu unakuta mfugaji anaingiza mifugo ambayo siyo tu inakula mazao lakini pia inaharibu mifereji ambayo imegharimiwa na Serikali,” alisema.

Alisema wafugaji wengi wanachojali wao ni ng’ombe kushiba na siyo uharibifu unaotokana na matendo yao. Bonde la Rukwa ni miongoni mwa maeneo nchini yaliyoathiriwa na uhamiaji wa wafugaji kutoka mikoa ya Mwanza na Shinyanga.

Akizungumzia ufanisi wa skimu hiyo, Waziri Mkuu aliwataka wakazi hao wahakikishe kuwa wanazalisha magunia 30 ya mpunga kwa kila ekari na magunia 20 – 25 kwa kila ekari ya mahindi ili kweda sambamba na mpango wa kuleta mapinduzi ya kilimo mkoani Rukwa (MAKIRU).

“Hii ni skimu ni nzuri na mmeanza na ekari 500 si haba ni mwanzo mzuri, lakini kikubwa na wakulima kuwasumbua mabwanashamba... mfuate umuulize nataka kupata magunia 30 ya mpunga kwa ekari moja nifanyeje? Vivyo hivyo, kwa wanaolima mahindi, mwambie bwana shamba nataka kuvuna magunia 25 katika eka yangu, nitumie njia gani?” alifafanua.
Aliwaonya wafugaji wanaopitisha mifugo yao kwenye barabara kwani kwa kufanya hivyo ni kuharibu miundombinu hiyo na pia ni kinyume cha sheria ya nchi.

“Ni sheria ya nchi inayokataza mifugo kupitishwa kwenye barabara lakini pia ni gharama sana kuzikarabati barabara hizi kila mwaka... ninawasihi sana msirihusu mifugo kupita katikati ya barabara, watengenezeeni njia zao huko pembeni.”

Alisema ukarabati wa barabara ya kutoka Ilemba hadi Mamba unaofanyika hivi sasa una nia ya kufungua bonde la Rukwa ili uzalishaji unaofanyika ulete tija kwa wakulima wa bonde hilo.

Aliwasisitizia haja ya kuwa na ghala ili waweze kuanzisha mfumo wa stakabadhi ya mazao ghalani ambapo mkulima huweka mazao yake katika na kulipwa wakati wa mavuno na SACCOS huku akisubiri bei ipande ili mazo hayo yauzwe na kupatiwa malipo mara ya pili kutokana namavuno yaleyale.

Katika harambee ya papo kwa papo kuchangia ujenzi wa ghala hiyo, Waziri Mkuu alichangisha sh. milioni 14.47 kutoka kwa wajumbe aliofuatana nao kwenye msafara wake na kuahidi kufuatilia ili kuhakikisha wanafanikiwa. Alimwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kuhakikisha wanaanza kujenga ghala hilo katika muda usiozidi miezi sita.

Mapema akisoma taarifa ya skimu hiyo, Bwana shamba wa skimu hiyo Bw. Zurubabeli Matimba alimweleza Waziri Mkuu kwamba skimu hiyo inakabiliwa na mmomonyoko wa udongo kutokana na mifugo inayoingizwa kwenye skimu hiyo kinyume cha taratibu.

Alisema changamoto nyingine inayowakabili ni uelewa mdogo miongoni mwa wakulima juu ya kilimo bora cha mpunga kwani wengi hutumia zaidi mbegu za asili ambazo hazikawii kuanguka upepo unapozidi.

Leo Waziri Mkuu anaanza ziara ya siku mbili katika jimbo lake la Mpanda Mashariki kwa kutembelea kata za Muze na Mamba ambako atafanya mikutano ya hadhara na kukabidhi kasiki ya kuhifadhia fedha kwa SACCOS ya Muze.


(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, MEI 12, 2009.

0 comments:

Post a Comment

About This Blog

Blog Archive

  © Blogger template Noblarum by Ourblogtemplates.com 2009

Back to TOP