MSAFARA WA WAZIRI MKUU WAKWAMA NJIANI MARA TATU

Wednesday, May 13, 2009

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

MSAFARA WA WAZIRI MKUU WAKWAMA NJIANI MARA TATU
*Ni kutokana na mvua na utelezi
*Aombwa na wananchi kupita barabara mbovu, akubali

MSAFARA wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda ulichelewa wa zaidi ya saa tatu kufika kwenye kijiji cha Muze katika bonde la Rukwa kwa sababu ya kukwama njiani mara tatu kutokana na utelezi.

Tukio lilitokea jana asubuhi (Jumanne, Mei 12, 2009) wakati akitoka Sumbawanga mjini kwenda kijijini hapo kukagua SACCOS ya Muze na kuzungumza na wananchi akiwa njiani kwenda Mamba, wilayani Mpanda kwa ziara ya siku mbili jimboni kwake.

Katika hali ya kawaida, safari ya kutelemka bonde la Rukwa ingechukua saa moja au pungufu ya hapo. Baadhi ya magari yaliyonasa katika utelezi huo ni gari la RPC, gari la walinzi na la Wasaidizi wa Waziri Mkuu.

Utelezi huo ulitokana na mvua zilizonyesha usiku wa kuamkia jana huku barabara aliyopita ya Ntendo hadi Muze ikiwa imemwagiwa kifusi ambacho kilikuwa kimeanza kusambazwa lakini hakijashindiliwa. Barabara hiyo ina urefu wa kilometa 37 lakini sehemu korofi ilikuwa na umbali wa kilometa 15.

Meneja wa TANROADS wa mkoa wa Rukwa, Eng. Joseph Nyamhanga alisema barabara hiyo ilikuwa inafanyiwa ukarabati wa awali ili iweze kufikia kiwango cha barabara zilizo chini ya Mradi wa Kuzikarabati Barabara ili zipitike muda wote (Performance Based Management and Maintenance of Roads – PMMR) ambao ni wa miaka mitano.

Alisema katika mpango huo, barabara ikishajengwa, inakuwa chini ya uangalizi wa mkandarasi mmoja kwa miaka mitano ambaye atapaswa kuifanyia matengenezo katika kipindi chote cha mradi. Mkandarasi anayejenga barabara hiyo ni KMM Entrepreneurs Ltd.)

Akizungumza baada ya kufika Mamba katika jimbo lake, Waziri Mkuu alisema Serikali inakabiliwa na changamoto kubwa ya kuufungua ukanda wa bonde la Rukwa ambao una kilometa za mraba 1,200 sawa na hekta 120,000 au ekari 300,000 ambazo zinatumika kuzalisha mazao mbalimbali kubwa likiwa mpunga na mahindi.

Alisema changamoto hiyo inakuwa ngumu zaidi kwa sababu ya milima ya Lyamba lya Mfipa ambayo inatenganisha bonde hilo na ukanda wa juu uliko mji wa Sumbawanga ambako kuna barabara kuu jambo linalowafanya wakulima na wafanyabiashara wapate taabu kusafirisha mazao hadi upande wa pili.

“Wakati tukishuka mlima huu, tumekuta magunia ya mpunga yakiwa yamelundikwa njiani kwa sababu malori (fuso) yanayosomba mizigo inabidi yabebe magunia machache yashushe njiani halafu yarudi tena bondeni kusomba mengine, yakimaliza yarudi kuchukua kidogo kidogo ule mzigo wa njiani ili yamalizie kupandisha mlima,” alisema.

Barabara nyingine zinazounganisha bonde hilo na ukanda wa juu ni za Miangalua – Kipeta yenye kilometa 60 na ya Kalambazite – Ilemba yenye kilometa 30 lakini zote zinapandisha mlima huo mkubwa wenye urefu wa mita 1,800 kutoka usawa wa bahari wakati bonde la ziwa Rukwa liko mita 800 kutoka usawa wa bahari.

Juzi, Waziri Mkuu alilazimika kupita barabara ya Kalambazite – Ilemba baada ya kuombwa na wakazi wa Sakalilo kufanya hivyo kwa sababu walimlalamikia kuwa wanalipa nauli ya sh. 10,000 kutoka Sumbawanga lakini wakifika kwenye mlima huo wanatelemeshwa kwenye mabasi na kuambiwa washuke kwa miguu.

Alisema ili barabara hizo ziwe na manufaa, itabidi zipandishwe daraja na kuwa za mkoa ili ziweze kuhudumiwa kikamilifu kwani hivi sasa hizo ziko chini ya Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ambayo haiwezi kumudu gharama za matengenezo.

Alisema katika miinuko mikali ambayo haizidi kilometa moja, barabara za mlima huo zitahitaji kuwekewa lami au zege katika maeneo korofi ili zisiendelee kuharibika na hivyo kuondoa kikwazo cha usafiri kwa wananchi waishio bondeni.

Changamoto nyingine inayolikabili bonde la Rukwa linaloanzia kata za Kipeta, Mtowisa hadi Majimoto ni ukosefu wa daraja katika mto Momba ambao unaunganisha wilaya za Sumbawanga, Rukwa na Mbozi, mkoani Mbeya. Baadhi ya wananchi waliiomba Serikali ijenge daraja kubwa kuliko lililopangwa kujengwa sasa ili magari ya mizigo yaweze kupita na kukuza biashara katika bonde hilo.

Leo Waziri Mkuu atafanya mikutano ya hadhara katika kata za Majimoto, Mbede, Usevya, Kashishi na Kibaoni kabla ya kurejea Mpanda Mjini. Anatarajiwa kurejea jijini Dar es salaam kesho mchana.


(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATANO, MEI 13, 2009.

0 comments:

Post a Comment

About This Blog

Blog Archive

  © Blogger template Noblarum by Ourblogtemplates.com 2009

Back to TOP